WAY

Tuesday, March 3, 2015

VIKONGWE WAUAWA MKOANI DODOMA KWA TUHUMA ZA USHIRIKINA ETI WANAZUIA MVUA ISINYESHE MAENEO YAO


     Kamanda wa Jeshi la Polisi Dodoma David Misime
Vikongwe watatu akiwemo mganga wa kienyeji Wilayani Kongwa Mkoani Dodoma, wameuawa kwa tuhuma za kuzuia mvua isinyeshe Wilayani humo.

Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na kamanda wa polisi mkoa wa Dodma, David Misime inasema kuwa tukio la kwanza lilitokea Machi mosi mwaka huu majira ya saa saba usiku katika kitongoji cha Golani, kijiji cha Masinyeti, kata ya Iduo, tarafa ya Mlali.

Kamanda amesema katika tukio hilo mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la Saidia Chakutwanga (80) ambaye ni mganga wa kienyeji aliuawa na watu waliojichukulia sheria mkononi kwa kupigwa na kitu kizito kichwani na kutobolewa macho.

Amesema uchunguzi wa awali unaonyesha chanzo cha mauaji hayo ni imani za kishirikina wakimtuhumu marehemu kuwa anazuia mvua kunyesha katika eneo hilo.

Katika tukio lingine amesema tarehe hiyo hiyo majira ya saa nane usiku kwenye kitongoji cha Majengo, kijiji cha Ihanda Kata na Tarafa ya Mlali mtu mmoja aliyemtaja kwa jina la Peter Kaluli (85) akiwa na mkewe aitwaye Kaila Kaluli (80) wakazi wa kitongoji cha Majengo wakiwa wamelala ndani ya nyumba yao ya tembe, waliuawa na watu wasiofahamika kwa kuangushiwa ukuta wa nyumba yao kisha kuchoma moto na kubomoa nyumba mbili za tembe.

“Watu hao walifanya uharibifu mwingine kwa kuwaua nguruwe mmoja na ng’ombe mmoja kumkata miguu ambao ni mali za marehemu hao,” alisema Misime.

Kwa mujibu wa Kmanda uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa chanzo cha mauaji na uharibifu huo ni imani za kishirikina wakiwatuhumu marehemu kuwa wanazuia mvua kunyesha.

Kutokana na tukio hilo watu wanne akiwemo Mwenyekiti wa Kijiji cha Ihanda na wazee wawili wa kimila wa kijiji wanashikiliwa na Polisi kuhusiana na tukio hilo kwani taarifa zinaonyesha waliandaa vikao vya kutekeleza mauaji hayo.

Upelelezi wa matukio yote mawili unaendelea ikiwa ni pamoja na kuwatafuta watuhumiwa wengine waliohusika na matukio haya ili sheri aiweze kuchukua mkondo wake.

Kufuatia tukio hilo Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Chiku Gallawa amewataka viongozi wa dini mkoani hapa kuhubiri amani kwa waumini wao ili vitendo vya mauaji kwa vikongwe viweze kukomeshwa.

0 comments:

Post a Comment

.

.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...