WAY

Monday, December 29, 2014

MIGOGORO YA ARDHI IMEANZA KULETA ATHARI ZA KIUCHUMI NA KIJAMII MIKOA YA KASKAZINI

                                 Mkuu wa wilaya ya siha Dk. Charles Mlingwa
Migogoro baina ya wafugaji na wawekezaji katika maeneo mbalimbali nchini, imeanza kuleta athari za kijamii na kiuchumi, baada ya taasisi za kielimu huko West Kilimanjaro, kulalamikia hatua ya usitishwaji wa huduma ya chakula mashuleni, pamoja na wasambazaji wa mazao kukosa soko kutokana na migogoro hiyo.

Kituo hiki kimelazimika kufuatilia moja ya mkasa uliojiri mwezi Novemba 2014 katika Ranchi ya Ndarakwai iliyopo Wilaya ya Siha Magharibi mwa Kilimanjaro ambapo athari za migogoro hiyo zinajionyesha wazi

Novemba 14 mwaka huu Kambi iliyopo ndani ya Ranchi ya Ndarakwai iligeuka majivu matupu pamoja na mali zingine kuharibiwa vibaya baada ya watu wanaodaiwa kuwa ni wafugaji kutekeleza mpango huu kwa madai ya kugombea malisho.

Uongozi wa Wilaya ya Siha kupitia kwa Mkuu wake wa Wilaya Dr.Charles Mlingwa unalitafsiri tukio hili kuwa la kihalifu ambalo limejiri baada mifugo ya vijiji vinavyozunguka Ranchi hiyo pamoja na maeneo ya Longido kuingizwa ndani ya Ranchi na baadaye askari kulazimika kuitoa kitendo kilichozua tafrani na baadaye wafugaji kulipiza kisasa kwa kuteketeza kambi ya mwekezaji.

Kituo hiki kimeangazia namna athari za mgogoro huu zinavyozikumba sekta zingine ambapo pia uongozi wa Ranchi umeeleza kusitisha mikataba ya wafanyakazi wake zaidi ya70 kutokana na janga hilo.

Shule ya Msingi Olmolok yenye wanafunzi mia nne ambayo ilikuwa ikinufaika na mpango wa chakula shuleni kutokana na uwekezaji katika Ranchi ya Ndarakwai sasa mpango huo umesitishwa na Mwalimu Mkuu wake msaidizi Betwel Mwasha anasema mahudhurio na kiwango cha taaluma vimeporomoka kwa kasi.

Mfanyabiashara wa Nyama katika kijiji cha Ngarenairobi Samwel Lizer aliyekuwa akisambaza kitoweo hicho kwa wanafunzi wa Shule ya Vetenari anasema mapato aliyokuwa akikusanya kwa kusambaza kilo 40 kila mwezi sasa yamesitishwa na hivyo kumsababishia hasara.

Katika Kijiji cha Miti Mirefu mfugaji mmoja wa kuku mama Julieta Baltazari aliyengia mkataba wa kusambaza mayai amebainisha kuathiriwa na mgogoro huo baada ya kusitishwa kwa mkataba.

Mkurugenzi Mkuuu wa Ranchi ya Ndarakwai Peter Jones anasema wameaua kusitisha huduma zote za kijamii kwa sasa kutokana na hasara iliyotokea baada ya nyumba ishrini ,magari sita pamoja na mali zingine zilizokuwa katika kambi yake kuteketezwa kwa moto na hivyo kufanya hasara inayofikia dola milioni moja..

Uwekezaji wa kipindi cha miaka 19 unaoendena na biashara ya utalii wa upigaji picha katika eneo hili lililo umbali wa kilometa 50 tokea katika hifadhi ya wanyama ya Amboseli nchini Kenya huwenda ukatoweka iwapo hakutakuwepo kwa hatua za dharura kumaliza mgogoro huu ambao ni taswira ya kile kinachojiri katika maeneo mbalimbali hapa nchini.

0 comments:

Post a Comment

.

.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...